Tuesday, April 7, 2009

MWENDELEZO WA MADA YA AINA MBALIMBALI ZA JUISI



Habari za siku chache wadau wenzangu. Bila shaka baadhi yenu mnajiandaa na Sikukuu ya PASAKA kwani ipo jirani sana. Napenda niseme maandalizi mema.
Leo nitaendeleza kuwapatia aina nyingine za juisi na kazi zake mwilini. Kumbuka, juisi ninazozungumzia hapa ni zile za matunda halisi, kwa wale wanaojua lugha ya wenzetu wanasema "Fresh fruit juice". Hapa sizungumzii juisi za madukani ambazo zimefungwa kwenye maboksi au chupa na wakazibatiza kuwa ni za matunda halisi kumbe ni mchanganyiko wa madawa au kemikali zenye ladha ya matunda. Ningependa nikushauri kuwa ni vema ukatumia matunda yetu yatokayo kule Lushoto, Chanika, Rufiji, Moshi, Mbeya na kwingineko ili kutengenezea juisi na unufaike kiafya. Huo ni ushauri wa bure lakini maamuzi unayo mwenyewe.
Haya tuangalie aina za juisi zifuatazo:
  • JUISI YA MCHANGANYIKO WA NDIZI NA CHUNGWA: Chukua ndizi kama mbili au zinazotosha kutengenezea kiasi cha juisi upendacho na chungwa au machungwa. Kisha osha vizuri matunda yako na menya ndizi halafu zikate vipande vidogo. Ndizi ninazozungumzia hapa ni ndizi mbivu na si vinginevyo. Weka vipande vya ndizi zako kwenye blenda kisha saga upate juisi yako. Chukua chungwa au machungwa na kamua ili upate juisi yake kisha changanya na saga kwa pamoja ili upate mchanganyiko ulio sahihi. Chukua maji safi na salama kama glasi moja kisha changanya. Unaweza kuweka sukari au asali kidogo ili kuleta ladha. Unaweza kuweka mchanganyiko wa juisi yako kwenye friji ili ipate ubaridi kidogo na iwe tayari kwa matumizi.
  • FAIDA ZA JUISI HII KIAFYA: Kumbuka tunda la ndizi lina madini ya potasiam na sodiam kidogo. Madini haya yana vitamini B na pia kuna magneziam ndani yake. Virutubisho vilivyomo vinasaidia mzunguko wa damu kwenye arteri kuwa mzuri. Pia katika mchanganyiko huu wa juisi kuna vitamini C na A.
  • Aidha juisi hii inasaidia kutunza na kuufanya moyo ufanye kazi yake vizuri na ina uwezo wa kuzuia shinikizo la damu (High Blood Pressure).
  • JUISI YA MCHANGANYIKO WA APPLE NA PARACHICHI: Chukua maparachichi na apple zinazotosha kutengeneza kiasi cha juisi yako. Osha vizuri matunda yako kwa usalama wa afya yako kisha menya na ondoa mbegu. Kata vipande vinavyoweza kusagika. Weka kwenye sahani au bakuli kisha saga kwenye blenda ili upate mchanganyiko sahihi. Unaweza kuchanganya na asali vijiko vikubwa vya chakula viwili au vitatu na maziwa kidogo. Weka kwenye friji ipate ubaridi kidogo.
  • FAIDA ZAKE KIAFYA: Virutubisho vilivyomo ndani ya matunda haya vina uwezo mkubwa wa kupunguza cholesterol kwenye damu hivyo kupunguza uwezekano mkubwa wa mtumiaji wa juisi hii kupatwa na magonjwa ya arteri/kuziba kwa mishipa ya damu. Aidha mchanganyiko huu unazuia magonjwa kama anaemia (ukosefu wa madini ya chuma na upungufu wa damu mwilini), kwani parachichi na apple vina viwango vikubwa vya madini ya chuma. Pia huzuia kansa ya colon.

Kumbuka matumizi ya juisi hizi ni ya mara kwa mara. Unapokunywa juisi kama hizi mara moja kwa mwezi haitokusaidia kitu. Pangilia juisi hizi kama sehemu ya mlo wako wa kila siku.

Kwa leo naishia hapo tutaendelea siku zijazo.

NAWATAKIENI MAANDALIZI MEMA YA SIKUKUU YA PASAKA NA PASAKA NJEMA.





Saturday, April 4, 2009

AINA MBALIMBALI ZA JUISI NA KAZI ZAKE MWILINI


Habari za siku wadau wa blog hii. Ni matumaini yangu kuwa mnaendelea vizuri katika shughulimbalimbali za kujitafutia riziki na maendeleo. Ningependa nikiri na kuwaomba radhi kwa ukimya wangu unaojitokeza mara kwa mara.



Leo nimeona nijibu baadhi ya maombi ya wasomaji wangu waliotaka kufahamu aina ya juisi mbalimbali na jinsi zinavyotengenezwa. Binafsi nimeona niwaongezee na kipengele kingine cha faida za juisi hizo katika mwili wa binadamu.

Zipo juisi za namna tofauti na matumizi yake yanategemea na malengo ya mtumiaji. Nadhani watumiaji wengi wanakunywa juisi bila kujua umuhimu au kazi yake mwilini. Wengi hawajui ni juisi gani itumike wakati gani.

Hebu fuatilia aina zifuatazo na upate kujua utengenezaji wake na kazi zake.

  • JUISI YA KAROTI NA APPLE: Chukua kiasi cha karoti na apple kinachotosha kutengeneza juisi kwa kiasi ulichokusudia. Usikose kipande cha limao kiasi cha nusu. Anza kuandaa juisi yako kwa kuosha na kumenya karoti na apple kisha katakata katika vipande vidogo vinavyoweza kusagika kirahisi kwenye blenda. Saga mchanganyiko wako ili upate juisi. Baada ya kupata mchanganyiko wa juisi yako kamulia limao kwa ajili ya kuongeza ladha. Unaweza kuiweka kwenye friji ili ipate ubaridi kidogo na tayari kwa kuinywa. Siyo lazima kuongeza sukari kwenye juisi kwani matunda yana sukari asilia.
  • JUISI YA KAROTI NA APPLE ina uwezo wa kutunza ngozi kwani tunda la apple linaondoa uchafu kwenye ngozi na karoti nayo kwa kutumia kirutubisho cha beta-karotini chenye uwezo wa kutengeneza Vitamin A hulinda na kurejesha uhai katika ngozi ambapo inaifanya ionekane nyororo. Pia juisi hii husafisha tumbo na kuondoa uchafu tumboni. Aidha juisi hii inafanya ini lifanye kazi yake vizuri kwa kulainisha nyongo na kusaidia kuondoa uchafu.

  • JUISI YA VIAZI MVIRINGO: Chukua viazi mviringo vinavyotosha kwa juisi. Andaa kwa kuviosha na kumenya kisha katakata vipande vidogo kwa ajili ya kuvisaga. Saga ili upate juisi uliyoikusudia.
  • JUISI YA VIAZI MVIRINGO inatumika kama dawa ya kuondoa au kupunguza asidi au gesi tumboni. Juisi ya viazi mviringo inaweza kusaidia kupunguza matatizo ya figo, kisukari, unene au kitambi.

  • JUISI YA MBOGAMBOGA: Juisi hii ina mchanganyiko wa mbogamboga kam vile karoti, nyanya na matango. Maandalizi yake ni kam juisi nyingine. Anza kwa kuosha kisha kumenya na kukatakata vipande. Saga mchanganyiko huo kwenye blenda ili upate juisi uliyoikusudia. Unaweza kuweka kwenye friji ili ipate ubaridi kidogo.
  • JUISI hii inasadaidia kuzuia kansa hasa ile ya kwenye mfumo wa kumeng`enya chakula, kukinga mapafu na artery. Pia inasaidia kuimarisha kinga.

  • JUISI YA TIKITI MAJI: Chukua tikiti maji (watermelon) na osha kisha likate vipande na chukua nyama yake ya ndani ambayo utaisaga na kupata juisi.
  • JUISI YA TIKITI MAJI ina uwezo wa kusafisha figo pamoja na njia ya mkojo. Inazuia unene kwa kuwa na kiwango kidogo cha calories.

KWA aina hizo chache za juisi unaweza kujua umuhimu wa juisi za matunda na mbogamboga tunazotumia. Kwa leo ninaishia hapo na siku zijazo nitaendelea kukupatia ufahamu kwa aina zingine za juisi pamoja na kazi zake.

SIKU NJEMA.