Tuesday, April 7, 2009

MWENDELEZO WA MADA YA AINA MBALIMBALI ZA JUISI



Habari za siku chache wadau wenzangu. Bila shaka baadhi yenu mnajiandaa na Sikukuu ya PASAKA kwani ipo jirani sana. Napenda niseme maandalizi mema.
Leo nitaendeleza kuwapatia aina nyingine za juisi na kazi zake mwilini. Kumbuka, juisi ninazozungumzia hapa ni zile za matunda halisi, kwa wale wanaojua lugha ya wenzetu wanasema "Fresh fruit juice". Hapa sizungumzii juisi za madukani ambazo zimefungwa kwenye maboksi au chupa na wakazibatiza kuwa ni za matunda halisi kumbe ni mchanganyiko wa madawa au kemikali zenye ladha ya matunda. Ningependa nikushauri kuwa ni vema ukatumia matunda yetu yatokayo kule Lushoto, Chanika, Rufiji, Moshi, Mbeya na kwingineko ili kutengenezea juisi na unufaike kiafya. Huo ni ushauri wa bure lakini maamuzi unayo mwenyewe.
Haya tuangalie aina za juisi zifuatazo:
  • JUISI YA MCHANGANYIKO WA NDIZI NA CHUNGWA: Chukua ndizi kama mbili au zinazotosha kutengenezea kiasi cha juisi upendacho na chungwa au machungwa. Kisha osha vizuri matunda yako na menya ndizi halafu zikate vipande vidogo. Ndizi ninazozungumzia hapa ni ndizi mbivu na si vinginevyo. Weka vipande vya ndizi zako kwenye blenda kisha saga upate juisi yako. Chukua chungwa au machungwa na kamua ili upate juisi yake kisha changanya na saga kwa pamoja ili upate mchanganyiko ulio sahihi. Chukua maji safi na salama kama glasi moja kisha changanya. Unaweza kuweka sukari au asali kidogo ili kuleta ladha. Unaweza kuweka mchanganyiko wa juisi yako kwenye friji ili ipate ubaridi kidogo na iwe tayari kwa matumizi.
  • FAIDA ZA JUISI HII KIAFYA: Kumbuka tunda la ndizi lina madini ya potasiam na sodiam kidogo. Madini haya yana vitamini B na pia kuna magneziam ndani yake. Virutubisho vilivyomo vinasaidia mzunguko wa damu kwenye arteri kuwa mzuri. Pia katika mchanganyiko huu wa juisi kuna vitamini C na A.
  • Aidha juisi hii inasaidia kutunza na kuufanya moyo ufanye kazi yake vizuri na ina uwezo wa kuzuia shinikizo la damu (High Blood Pressure).
  • JUISI YA MCHANGANYIKO WA APPLE NA PARACHICHI: Chukua maparachichi na apple zinazotosha kutengeneza kiasi cha juisi yako. Osha vizuri matunda yako kwa usalama wa afya yako kisha menya na ondoa mbegu. Kata vipande vinavyoweza kusagika. Weka kwenye sahani au bakuli kisha saga kwenye blenda ili upate mchanganyiko sahihi. Unaweza kuchanganya na asali vijiko vikubwa vya chakula viwili au vitatu na maziwa kidogo. Weka kwenye friji ipate ubaridi kidogo.
  • FAIDA ZAKE KIAFYA: Virutubisho vilivyomo ndani ya matunda haya vina uwezo mkubwa wa kupunguza cholesterol kwenye damu hivyo kupunguza uwezekano mkubwa wa mtumiaji wa juisi hii kupatwa na magonjwa ya arteri/kuziba kwa mishipa ya damu. Aidha mchanganyiko huu unazuia magonjwa kama anaemia (ukosefu wa madini ya chuma na upungufu wa damu mwilini), kwani parachichi na apple vina viwango vikubwa vya madini ya chuma. Pia huzuia kansa ya colon.

Kumbuka matumizi ya juisi hizi ni ya mara kwa mara. Unapokunywa juisi kama hizi mara moja kwa mwezi haitokusaidia kitu. Pangilia juisi hizi kama sehemu ya mlo wako wa kila siku.

Kwa leo naishia hapo tutaendelea siku zijazo.

NAWATAKIENI MAANDALIZI MEMA YA SIKUKUU YA PASAKA NA PASAKA NJEMA.





Saturday, April 4, 2009

AINA MBALIMBALI ZA JUISI NA KAZI ZAKE MWILINI


Habari za siku wadau wa blog hii. Ni matumaini yangu kuwa mnaendelea vizuri katika shughulimbalimbali za kujitafutia riziki na maendeleo. Ningependa nikiri na kuwaomba radhi kwa ukimya wangu unaojitokeza mara kwa mara.



Leo nimeona nijibu baadhi ya maombi ya wasomaji wangu waliotaka kufahamu aina ya juisi mbalimbali na jinsi zinavyotengenezwa. Binafsi nimeona niwaongezee na kipengele kingine cha faida za juisi hizo katika mwili wa binadamu.

Zipo juisi za namna tofauti na matumizi yake yanategemea na malengo ya mtumiaji. Nadhani watumiaji wengi wanakunywa juisi bila kujua umuhimu au kazi yake mwilini. Wengi hawajui ni juisi gani itumike wakati gani.

Hebu fuatilia aina zifuatazo na upate kujua utengenezaji wake na kazi zake.

  • JUISI YA KAROTI NA APPLE: Chukua kiasi cha karoti na apple kinachotosha kutengeneza juisi kwa kiasi ulichokusudia. Usikose kipande cha limao kiasi cha nusu. Anza kuandaa juisi yako kwa kuosha na kumenya karoti na apple kisha katakata katika vipande vidogo vinavyoweza kusagika kirahisi kwenye blenda. Saga mchanganyiko wako ili upate juisi. Baada ya kupata mchanganyiko wa juisi yako kamulia limao kwa ajili ya kuongeza ladha. Unaweza kuiweka kwenye friji ili ipate ubaridi kidogo na tayari kwa kuinywa. Siyo lazima kuongeza sukari kwenye juisi kwani matunda yana sukari asilia.
  • JUISI YA KAROTI NA APPLE ina uwezo wa kutunza ngozi kwani tunda la apple linaondoa uchafu kwenye ngozi na karoti nayo kwa kutumia kirutubisho cha beta-karotini chenye uwezo wa kutengeneza Vitamin A hulinda na kurejesha uhai katika ngozi ambapo inaifanya ionekane nyororo. Pia juisi hii husafisha tumbo na kuondoa uchafu tumboni. Aidha juisi hii inafanya ini lifanye kazi yake vizuri kwa kulainisha nyongo na kusaidia kuondoa uchafu.

  • JUISI YA VIAZI MVIRINGO: Chukua viazi mviringo vinavyotosha kwa juisi. Andaa kwa kuviosha na kumenya kisha katakata vipande vidogo kwa ajili ya kuvisaga. Saga ili upate juisi uliyoikusudia.
  • JUISI YA VIAZI MVIRINGO inatumika kama dawa ya kuondoa au kupunguza asidi au gesi tumboni. Juisi ya viazi mviringo inaweza kusaidia kupunguza matatizo ya figo, kisukari, unene au kitambi.

  • JUISI YA MBOGAMBOGA: Juisi hii ina mchanganyiko wa mbogamboga kam vile karoti, nyanya na matango. Maandalizi yake ni kam juisi nyingine. Anza kwa kuosha kisha kumenya na kukatakata vipande. Saga mchanganyiko huo kwenye blenda ili upate juisi uliyoikusudia. Unaweza kuweka kwenye friji ili ipate ubaridi kidogo.
  • JUISI hii inasadaidia kuzuia kansa hasa ile ya kwenye mfumo wa kumeng`enya chakula, kukinga mapafu na artery. Pia inasaidia kuimarisha kinga.

  • JUISI YA TIKITI MAJI: Chukua tikiti maji (watermelon) na osha kisha likate vipande na chukua nyama yake ya ndani ambayo utaisaga na kupata juisi.
  • JUISI YA TIKITI MAJI ina uwezo wa kusafisha figo pamoja na njia ya mkojo. Inazuia unene kwa kuwa na kiwango kidogo cha calories.

KWA aina hizo chache za juisi unaweza kujua umuhimu wa juisi za matunda na mbogamboga tunazotumia. Kwa leo ninaishia hapo na siku zijazo nitaendelea kukupatia ufahamu kwa aina zingine za juisi pamoja na kazi zake.

SIKU NJEMA.





Thursday, February 26, 2009

KARIBUNI TENA WADAU

Habari za siku nyingi wadau wa blog hii maridhawa. Kwa vile tangu mwaka wa 2009 uanze hatujawasiliana kwa namna moja au nyingine ningependa kuwatakia HERI YA MWAKA MPYA WA 2009. Nasema karibuni tena kwani ni kipindi kirefu nilikuwa sipo hewani kuwapatia vitu vizuri kwa ajili ya kuilinda afya yako.

Nawaomba radhi wadau wenzangu kwani nilitoweka ghafla bila kuwapa taarifa yeyote huku wengine mkijiuliza mwaswali yasiyo na majibu juu ya uwepo wangu hapa duniani. Labda niwaondoe wasiwasi kuwa mie nipo salama salimini na afya isiyo na mgogoro. Isipokuwa mambo fulani yalinifanya nikae kando bila kutoa mada yeyote katika safu ya blog hii.
Kwa sasa nimerejea kwa kasi ile ile. Maana sipendi kuwaongopea eti kasi mpya kwani wengi wetu hatujui hiyo kasi mpya inakuwaje kwa sababu imeonekana kutuletea madhara badala ya furaha.
Wakati wowote kuanzia sasa wadau mtaanza tena kupata ile elimu juu ya afya zetu kwa kutumia mazao asilia kama ilivyokuwa awali. Tutakiane afya njema ili tuweze kutimiza malengo yetu.
KARIBUNI SANA

Thursday, September 18, 2008

UPUNGUFU WA NGUVU ZA KIUME (SEXUAL IMPOTENCE)

Hongera kwa saumu kwa wale waliofunga, na wale wenzangu na mie habari za siku tele. Ndugu zangu msidhani kama niliingia mitini bali dharura za kimaisha zilinizonga. Leo naomba nizungumzie kuhusu suala nyeti la upungufu wa nguvu za kiume na namna ambavyo mtu mwenye tatizo kama hili anaweza kutumia ushauri wangu ili kurejesha heshima yake katika kufanya mambo ya kikubwa. Hapo awali inasemekana tatizo hili lilisababishwa na sababu za kisaikolojia pamoja na uzee au umri mkubwa ambapo viungo vya mwili vinakuwa vimechoka.
Kwa miaka ya hivi karibuni imebainika kuwa sababu zinazosababisha upungufu wa nguvu za kiume zimeongezeka na zifuatazo ni baadhi ya sababu hizo, nazo ni;
  • Kutokana na mabadiliko ya kisayansi na kukua kwa teknolojia wanaume wengi wamekuwa wakiishi maisha rahisi ya kutotumia miili yao kwa kufanya kazi zinazotumia nguvu na matokeo yake mwili unashindwa kujenga misuli imara katika viungo mbalimbali vya mwili.
  • Ulaji wa vyakula vilivyopitia viwandani na vyenye asili ya mafuta na protini nyingi ambapo vyakula hivyo vinakosa virutubisho muhimu kwa ajili ya kuimarisha viungo nyeti. Vyakula vyenye asili ya mafuta vinasababisha kuwepo kwa cholestral kwenye damu ambayo inapunguza au kuzuia mzunguko wa damu kwenye nyeti za mwanaume na hatimaye kushindwa kufanya kazi vizuri.
  • Matumizi ya mara kwa mara ya vileo/pombe, kahawa, uvutaji wa sigara nayo yanachangia upungufu wa nguvu za kiume.
  • Athari za magonjwa kama kisukari, arteri, magonjwa ya neva yanayosababishwa na ulaji wa vyakula vyenye protini nyingi na mafuta mengi.
  • Ukosefu wa madini na vitamini mbalimbali zinazopatikana kwa wingi kutoka kwenye matunda na mbogamboga.

Kutokana na kero ya tatizo la upungufu wa nguvu za kiume au uhanithi, watu wengi wamekuwa wakijaribu kutumia vidonge ili waweze kuongeza nguvu na kufurahia tendo la ndoa. Imebainika kuwa matumizi ya vidonge hivyo yana madhara kwa afya ya mtumiaji. Baadhi ya athari anazoweza kuzipata mtumiaji wa dawa hizo ni pamoja na kuharisha, kichefuchefu, kuumwa na kichwa, kupooza baadhi ya viungo, upofu, kutosikia, na hata kupoteza kabisa kwa nguvu za kiume. Hali hiyo imewafanya watu wengi siku hizi wageukie matumizi ya dawa za mimea asilia au vyakula asilia ambapo havina athari kwa mtumiaji.

Hivyo basi mtu mwenye tatizo la uhanithi au upungufu wa nguvu za kiume anapaswa kuzingatia yafuatayo:

  • Kutumia kwa wingi matunda ikiwa kama sehemu ya mlo wake kila wakati anapopata mlo kwa siku tano hadi saba za mwanzo. Mtumiaji anaweza kuwa na milo mitatu kwa siku ambapo pia matumizi ya juisi ya zabibu, machungwa, apple, peas, nanasi, parachichi na tikitiki maji yanahimizwa.
  • Matumizi ya vyakula vya nafaka pia yanafufua matumaini kwa mtu aliyepoteza uweza wa kufanya tendo la ndoa kuweza kusimama upya. Inashauriwa pia mtumiaji atumie asali, mtindi, kitunguu saumu, mbogamboga na matunda mara kwa mara. Wakati huo huo mgonjwa aepuke matumizi ya sigara, pombe au vileo, kahawa, na vyakula vilivyopitia viwandani na vyenye protini na mafuta mengi.
  • Mazoezi ya viungo au mwili ama kufanya kazi zinazotumia nguvu nako kunasaidia kuimarisha viungo vya mwili. Iwapo mgonjwa atafanya kazi ya kutumia nguvu au mazoezi ya viungo japo dakika 30 hadi 45 kila siku na kisha kula vyakula vilivyoelezewa hapo juu anaweza kuwa na uwezo wa kusimama mwenyewe pasipo kutumia msaada wa vidonge vya kuongeza nguvu.

Pamoja na hayo machache mada ijayo nitaendeleza kutaja baadhi ya vyakula, matunda na matumizi ya mbogamboga na kazi zake katika kufufua uwezo wa wanaume aliyepoteza nguvu za kiume.

KILA LA KHERI.

2Flag.

Wednesday, September 10, 2008

SAMAHANI WANABLOG

Napenda kuwaomba samahani wanablog kwasababu nimekuwa kimya kwa muda sasa. Sababu mojawapo ni kwamba kwa kipindi kisichopungua wiki moja iliyopita nilikuwa na dharura kiasi ambacho nimeshindwa kuwawekea matoleo mapya kwenye blog hii. Hata hivyo, hali hiyo inaweza kuendelea kwa siku kadhaa na pindi nitakapomaliza dharura zangu nitaendelea kuwapatia mada mbalimbali kama kawaida. Naomba uvumilivu wenu, tafadhali.

2flag.

Wednesday, September 3, 2008

JINSI YA KUPUNGUZA UNENE


Za leo! Mambo vipi! Hizi ndizo salamu za siku hizi hasa kwa vijana. Baada ya salamu hiyo naomba turudi kwenye mada ya leo ya jinsi ya kupunguza unene. Kwanza kabisa napenda kuwashauri watu wanene wasitumie vidonge/madawa ya kiwandani kwa lengo la kupunguza unene, kwani vidonge vina athari zake mwilini ukizingatia kuwa vina kemikali ambazo baadhi hubakia mwilini na kutengeneza sumu.


Watu wanashauriwa kutumia vitamini itokanayo na matunda na mbogamboga. Aidha, kwa mtu mnene kushinda na njaa siyo dawa au tiba sahihi ya kupunguza unene. Mtu anayetaka kupunguza unene/uzito ni vema akazingatia misingi ifuatayo:



  • Punguza kula chumvi nyingi maana chumvi inatunza maji mwilini ambayo pia yana mchango mkubwa katika kuongeza uzito wa mwili. Kwa kuacha kula chumvi nyingi maji yataweza kupungua mwilini kwa njia ya mkojo au jasho.


  • Ongeza kula vyakula vyenye madini ya potasium, calcium, na magnesium ambapo madini hayo yanapatikana kutoka kwenye mbogamboga mbichi na matunda au maziwa ya soya.


  • Kula vyakula vyenye wanga, punguza vyakula vyenye mafuta na protini.


  • Kunywa maji mengi kiasi cha lita 2 kwa siku na kwa kila siku.


  • Fanya mazoezi ya mwili/viungo japo kwa dakika 30 hadi 60 kila asubuhi. Kutembea ni mojawapo ya mazoezi.

Katika kuongezea vitu hivyo hapo juu, mlengwa anashauriwa pia kutumia;




  • Asali kijiko kimoja na kuchanganya nusu ndimu au limao kwenye maji yenye uvuguvugu kiasi cha glasi moja na kunywa mara kwa mara.


  • Matumizi ya cabbage pia yamethibitika kuwa na mchango mkubwa katika kupunguza unene kwani kemikali zilizomo ndani yake zinasaidia kuzuia wanga na sukari kubadilishwa kimfumo na kuwa mafuta ambayo ndicho chanzo cha unene wa mwili.


  • Ulaji wa nyanya fresh kati ya moja au mbili kila siku asubuhi kama kifungua kinywa kwa miezi kadhaa nako kunachangia kupunguza unene, na ni njia salama sana ya kupunguza unene.


  • Kunywa glasi mbili za maji ya uvuguvugu kila siku asubuhi mara baada ya kuamka kunasaidia kupunguza unene.

Aidha mtu mnene anaweza kutumia diet rahisi ifuatayo ili kupunguza unene;




  1. Asubuhi, kunywa juisi ya matunda fresh au kula matunda na kipande cha mkate usiopakwa siagi.


  2. Mchana, kula vegetable salad na slice 2 za mkate pamoja na matunda au juisi.


  3. Usiku, kula fruit salad au supu ya mbogamboga.

Hakikisha ratiba hiyo inafuatwa kila siku na acha kabisa kutumia vyakula vingine vyenye asili ya mafuta kama vile nyama.


Nadhani kwa hayo machache yanaweza kusaidia. Nimeona niwawekee diet ambayo ni rahisi kupatikana na kutengeneza kwa gharama nafuu.


Asante.


2flag.

Tuesday, September 2, 2008

SIJUI KWA NINI NINAKUWA MNENE WAKATI NINAKULA KIDOGO


Jamani habari za kushinda au kushindwa! Nasema hivyo kwani siyo watu wote wanaoshinda bali wapo walio wengi katika kasi hii wanashindwa ila hawana mahali pa kulalamikia.


Leo ninakuja na ile mada yetu juu ya unene, kitambi au kuwa na uzito mwingi mwilini. Wapo watu ambao wamekuwa wakilalamika na kusema kuwa " Jamani hata sijui kwa nini ninakuwa mnene wakati ninajitahidi kula kidogo au kujinyima mlo wa mchana pamoja na kufanya mazoezi". Watu wengi wanadhani kula sana ndiyo kunasababisha unene. Kumbe, hicho pekee siyo chanzo cha tatizo. Kwani miongoni mwetu tunawajua watu wembamba ambao wanakula sana lakini wanabaki na wembamba wao. Wengine wamekuwa wakila sana ili kuutafuta unene lakini hawanenepi.


Hivyo, licha ya chakula zipo sababu zingine zinazosababisha unene kwani wataalamu mbalimbali wamejaribu kutafiti chanzo cha unene lakini wameshindwa kupata jibu sahihi. Siyo watu wote wanaopata unene kwa kula vyakula, na sababu ya tofauti hizo bado kujulikana. Zifuatazo ni baadhi ya vyanzo vya unene:



  1. Kurithi: Wapo watu ambao wamerithi unene kutoka kwa mababu au wazazi ambapo kunakuwa na uhusiano fulani wa kizazi hicho unaofanana na ulaji wa vyakula fulani. Mtoto ambaye wazazi wake ni wanene ana uwezekano wa asilimia 80 ya yeye pia kuwa mnene kwani inasadikika kuwa hata yeye atakula kama wazazi wake.


  2. Sababu binafsi: Hii inatokana na sababu za kihomoni ambapo zipo homoni mwilini zinazochangia kuzalishwa kwa mafuta kwa wingi mwilini ambayo yanasababisha unene.


  3. Hupungufu wa joto mwilini: Inasemekana kuwa watu wanene wana joto kidogo mwilini kitu kinachochangia kutokutumika vizuri kwa calories zilizozalishwa mwilini, kwani calories zisizotumika zinabadilishwa na kuwa mafuta ambayo ndiyo chanzo cha unene. Joto jingi mwilini linasaidia kuchoma vizuri calories na kufanya mwili kukosa kutengeneza akiba ya mafuta. Kinyume na watu wanene, watu wembamba wanasemekana kuwa na joto jingi linalochoma vizuri calories na kuzifanya zitumike vizuri pasipo kubaki akiba ya mafuta mwilini. Ndiyo maana watu wanene wanashauriwa kufanya mazoezi ili kuzalisha joto la kutosha mwilini ili kuchoma akiba ya mafuta iliyopo mwilini.


  4. Kuhisi njaa mapema na kuwa na hamu ya kula: Inasemekana watu wanene wanahisi njaa mapema na wanakuwa na hamu ya kula ili kuponya njaa yao tofauti na watu wembamba. Aidha miili mikubwa inahitaji chakula kingi ili kutosheleza mahitaji ya miili hiyo.


  5. Uvivu: Pia imebainika kuwa watu wanene ni wavivu wa kufanya shughuli zinazotumia nguvu nyingi ikiwamo mazoezi. Hali hiyo inawafanya waendelee kuhifadhi akiba nyingi ya mafuta mwilini yanayoongeza unene.

JE KIFANYIKE NINI ILI KUONDOKANA NA HALI YA UNENE?


Ungana nami katika mwendelezo wa mada hii.


ASANTE.


2FLAG