Monday, September 1, 2008

KAZI YA VIRUTUBISHO VYA KAROTI


Kama tulivyotangulia kuona zao la karoti na matumizi yake, leo nitaelezea japo kwa ufupi kazi ya virutubisho vinavyopatikana kwenye zao hilo. Virutubisho hivyo ni vifuatavyo:



  1. Vitamini A (Beta - Carotene); hii ni vitamini inayotokana na kirutubisho kinachojulikana kama beta - carotene ambapo mwili hukibadilisha kuwa vitamini A pindi kiingiapo mwilini. Kazi kubwa ya kirutubisho hiki ni kutengeneza retina, kiungo ambacho kipo ndani ya jicho ambapo jicho linapewa uwezo wa kuona vizuri hasa kwenye mwanga hafifu. Kwa wale wenye matatizo ya kuona gizani, yaani night blindness wanashauriwa kula karoti kwa wingi. Pia kirutubisho hiki kinasaidia kutengeneza chembe (cell) kwa ajili ya ngozi, kinywa, macho, na viungo vingine laini ndani ya mwili. Aidha beta - carotene hupunguza uwezekano wa mwili kupatwa na magonjwa ya kansa kwa kuwa na uwezo mkubwa wa kupigana na magonjwa ya aina hiyo. Inasemekana kuwa wavutaji wa sigara wanaokula karoti kwa wingi wanapunguza uwezekano wa kupatwa na magonjwa ya kansa kwenye mapafu kuliko wale ambao wanakula kidogo au hawali kabisa.


  2. Fiber, hii inasaidia kulainisha choo na hata kukinga kuta za utumbo.


  3. Kuna kitu kinaitwa essential oil ambapo kazi yake kubwa ni kupigana na vijidudu tumboni.

Hivyo basi, ulaji wa karoti unaweza kuboresha afya yako na kujikinga na maradhi mbalimbali ambayo yanaweza kukugharimu pindi unapoyapata. Ni vema ukajijengea tabia ya kula karoti japo moja kwa siku, kwani zinapatikana kwa urahisi kabisa na ni kwa pesa kidogo tu.


Mada ijayo nitajibu maombi ya wadau waliotaka niwapatie japo ushauri wa kupunguza vitambi vyao ambavyo leo vimekuwa kero kwao na kusababisha washindwe kufanya kazi nyingine kwa umahiri kabisa.


KILA LA HERI, TUONANE SIKU HIYO, MUNGU AKIPENDA.


2FLAG.



No comments: